Idadi ya vifo katika kisiwa cha Hawaii nchini Marekani imefikia watu 93
Idadi ya vifo kufuatia moto wa nyika katika kisiwa cha Hawaii nchini Marekani imefikia watu 93. Huo ndio mkasa mkubwa zaidi wa moto wa nyika kuwahi kutokea Marekani katika zaidi ya karne moja
Maafisa wa Kaunti ya Maui wamesema idadi ya vifo inatarajiwa kuongezeka baada ya mbwa waliopewa mafunzo ya kunusa na kugundua iliko miili kujumuishwa katika shughuli za kutafuta miili kwenye vifusi.
Kiwango cha uharibifu kinaendelea kuonekana ikiwa ni siku tano baada ya moto huo mkubwa kuteketeza mji wa kitalii wa Lahaina, na kuyateketeza majengo na magari. Gavana wa Hawaii Josh Green ameonya kuwa idadi ya vifo huenda itaendelea kuongezeka huku waathirika zaidi wakipatikana. Mamia ya watu bado hawajulikani waliko kufuatia mkasa huo wa moto wa nyika.
Moto huo unafuatia matukio mengine mabaya ya hali ya hewa Amerika ya Kaskazini wakati wa majira ya sasa ya joto, huku mioto ya nyika iliyovunja rekodi ikiwa bado inawaka Canada na wimbi kubwa la joto linaloikumba sehemu ya kusini magharibi mwa Marekani.
Ulaya na maeneo mengine ya Asia pia yameshuhudia kupanda kwa viwango vya joto.
Source Credit:Dw