Kifo cha Prof. William Mahalu Mwasisi na Daktari Bingwa wa upasuaji wa moyo hapa nchini
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Prof. William Mahalu aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo na mmoja wa madaktari bingwa wa moyo wa kwanza hapa nchini.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu akiwa jijini Arusha Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt. Peter Kisenge alisema Prof. Mahalu alikuwa amelazwa JKCI kwaajili ya matibabu na alifariki usiku wa tarehe 20/08/2023.
Dkt. Kisenge alisema Prof. Mahalu ni miongoni mwa madaktari bingwa wa kwanza watatu wa moyo nchini ambao jitihada zao ziliwezesha kuanzishwa kwa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kupatikana kwa matibabu ya kibingwa ya moyo nchini Tanzania.
“Kifo cha Prof.Mahalu ni pigo kubwa kwa Taasisi yetu licha ya kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya JKCI pia alikuwa daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu na mshauri mzuri katika kutekeleza majukumu yetu hii ni kutokana na uzoefu wake wa muda mrefu aliokuwa nao,”.
“Tumempoteza mwasisi wa upasuaji wa moyo hapa nchini, ni pigo kubwa kwetu sisi wataalamu wa magonjwa ya moyo kwani kupitia Prof. Mahalu wataalamu wengi wa afya walivutiwa kujiendeleza na kuwa madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo hapa nchini”, alisema Dkt. Kisenge.
Kwa upande wake daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI)
Evarist Nyawawa alisema alimfahamu Prof.William Mahalu kuwa ni mmoja wa madaktari wa kwanza kabisa katika kusomea fani ya upasuaji wa moyo hapa nchini ambaye ni mzalendo kwani alipohitimu mafunzo yake ya upasuaji nchini Uingereza alirudi Tanzania na kutaka kuanzisha upasuaji wa moyo lakini kulingana na vipaumbele vya serikali kwa kipindi hicho hakuweza kufanya upasuaji huo na kwenda nchini Zimbabwe.
Dkt. Nyawawa alisema mara baada ya serikali kutia mkazo wa kutaka kuanzisha upasuaji wa moyo ikawachagua wataalamu 26 na kuwapeleka nchini India kujifunza upasuaji wa moyo wa fani mbalimbali na mara baada ya kurudi Prof. Mahalu kwa uzalendo wake alirejea nchini ili kujumuika nao na kuanza kufanya upasuaji wa moyo katika chumba cha upasuaji cha Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI).