Kambi Maalumu ya Upimaji na Matibabu ya Moyo Yatua Dar es Salaam
Wakazi wa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani wametakiwa kujitokeza kwa wingi katika zoezi la upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo linalofanyika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group.
Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati akizungumza na wananchi waliofika katika zoezi la upimaji na matibabu ya moyo linalofanyika katika kambi maalumu ya siku mbili inayofanyika JKCI Hospitali ya Dar Group.
Dkt. Kisenge alisema wananchi wakipata mapema huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo wataisaidia Serikali kupunguza gharama za kulipia matibabu hayo kwani matibabu ya kibingwa ikiwemo upasuaji wa moyo gharama zake ni kubwa.
“Hadi sasa watu 84 wameshapata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo na wengi tuliowaona wanamatatizo ya shinikizo la juu la damu, huu ni ugonjwa ambao tumekuwa tukiwakuta nao wananchi wengi tunaowaona katika maeneo mbalimbali hapa nchini”, alisema Dkt. Kisenge.
Dkt. Kisenge alisema magonjwa ya moyo yamekuwa yakiongoza kwa kuua watu wengi hapa Duniani ambapo kwa takwimu za Shirika la Afya Dunia (WHO) watu milioni 17 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na magonjwa hayo.
“Taasisi yetu imeamua kusogeza upatikanaji wa huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa kuwafuata wananchi mahali walipo, tunahitaji wananchi wenye matatizo ya moyo wapate huduma za matibabu mapema”,.
“Huduma hii inajulikana kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services tunawafuata wananchi mahalli walipo na kutoa huduma za uchunguzi na upimaji wa magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo ya moyo na kisukari pia tunatoa ushauri wa jinsi ya kuepukana na magonjwa haya pamoja na elimu ya lishe bora”, alisema Dkt. Kisenge.
Kwa upande wao wananchi waliopata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo waliishukuru Serikali kwa huduma waliyoipata na kuomba Taasisi hiyo kutoa huduma hiyo mara kwa mara kwani wengi wao inawawia vigumu kwenda moja kwa moja JKCI kupata matibabu hii ni kutokana na utaratibu uliopo wa kupata rufaa.