Issa Juma, Kaka yake Waziri Mkuu Kassim Majaliwa azikwa Ruangwa
Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dkt. Doto Biteko ameungana na Viongozi mbalimbali wa kitaifa na Watanzania kwa kutoa salamu za pole kwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa kufuatia kifo cha Kaka yake, marehemu Issa Juma, aliyezikwa leo.
Akiongea November 06, 2023 Wilayani Ruangwa Mkoa wa Lindi wakati akitoa salamu hizo kwa niaba ya Mawaziri, Dkt. Biteko amesema Watanzania wanaupendo wa dhati kwa Waziri Mkuu Majaliwa ambao wameuonesha pia katika kipindi hichi cha kumpoteza marehemu Kaka yake.
“Sisi ni kielelezo kuwa Watanzania wana upendo nawe ndio maana tumekuja kuungana pamoja na wewe, kulia pamoja na wewe lakini kukutia moyo kwamba sisi tuliofika hapa na wengine tunakupa pole kwa msiba wa kumpoteza Kaka”
Amesema kuwa, jambo lolote linalotokea ni mipango ya Mwenyezi Mungu hivyo ni muhimu kuombeana heri ili tuwe na mwisho mwema duniani.
Kwa upande wake, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amewashukuru Watanzania kwa kumfariji katika kipindi hichi cha msiba wa Kaka yake ambapo amesema amepokea salamu za pole kutoka kwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Zanzibar, Dkt.Hussein Mwinyi na Watanzania wote wanaompa pole na kumfariji.