Muimbaji wa nyimbo za Injili Ivy Kombo na mume wake wakamatwa kwa kuwa na shahada feki za sheria
Muimbaji wa nyimbo za Injili Ivy Kombo na mume wake wakamatwa kwa kuwa na shahada feki za sheria.
Mwanamuziki wa nyimbo za Injili kutoka Zimbabwe, Ivy Kombo na mumewe, Mchungaji Admire Kasi wametiwa mbaroni kwa tuhuma za kujipatia vyeti feki kwa njia ya udanganyifu nchini humo.
Gazeti la Herald liliripoti kuwa kukamatwa kwao kulifanywa na wachunguzi wa Tume ya Kupambana na Rushwa ya Zimbabwe (ZACC), ambao walifichua maelezo ya kutatanisha yanayohusu sifa zao za kisheria.
Kukamatwa kwa Ivy Kombo na mumewe, Mchungaji Admire Kasi kulikuja miezi michache tu baada ya kutangazwa kama mawakili. Inadaiwa walipata vyeti vyao kupitia usaidizi wa afisa aliyesimamishwa kazi kutoka Baraza la Elimu ya Sheria.
Ivy Kombo alidai kuwa ana shahada ya Sheria ya LLB na Sheria ya Biashara ya Kimataifa ya LLM kutoka Chuo Kikuu cha Bedfordshire nchini Uingereza. Wakati mumewe ana Shahada ya Uzamili ya Sheria kutoka Chuo Kikuu cha Buckingham (Uingereza).
Wanandoa hao walifikishwa mbele ya Mahakama ya Harare mchana wa jana kwa mashtaka ya ulaghai na kutoa ushahidi wa uwongo.