Watengeneza Biskuti za Bangi wakamatwa, biskuti zinachanganywa na bangi aina ya skanka
Watengeneza Biskuti za Bangi wakamatwa, biskuti zinachanganywa na bangi aina ya skanka
Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA) imewakamata Watu 16 wanaojihusisha na shughuli za utengenezaji wa biskuti kwa kuchanganya na bangi aina ya skanka katika eneo la Kawe Jijini Dar es Salaam ambapo Watu sita wamefikishwa Mahakamani na 10 watafikishwa Mahakamani taratibu za kisheria zikikamilika
Akiongea leo November 08,2023 Jijini Dar es salaam, Kamishna Jenerali wa DCEA Aretas James Lyimo amesema Watuhumiwa hao wamekutwa wakiendelea na uzalishaji wa biskuti hizo kwa kutumia mtambo mdogo wa kusaga skanka na vifaa vya kutengenezea biskuti za bangi.
“Skanka ni jina la mtaani linaloitambulisha aina ya bangi yenye kiwango kikubwa cha sumu ya TetraHydroCannabinol THC, skanka ina sumu zaidi ya asilimia 45 ikilinganishwa na asilimia 3 hadi 10 zilizo katika bangi ya kawaida, hivyo skanka ina madhara makubwa zaidi kwa Mtumiaji ikiwemo kuamsha matatizo ya afya ya akili”