Aliyesema mwezie ana HIV alipa faini ya Mil.14.7 Nchini Kenya
Mahakama nchini Kenya imeamuru Mwanaume mmoja aliyepewa jina la FO (Sio jina lake halisi) kulipa Ksh 850,000 (Tsh. mil 14.7) kama fidia ya uharibifu alioufanya kutokana na kuanika hali ya Virusi vya UKIMWI vya Rafiki yake kwa kutangaza kuwa mwenzake ana UKIMWI kupitia group la WhatsApp na kusababisha Mtu huyo kunyanyapaliwa.
Uamuzi huo umetolewa na Mahakama inayojulikana kama ‘HIV and AIDS Tribunal’ ambayo ni chombo pekee cha kisheria duniani chenye mamlaka ya kutoa kuhukumu ya kesi zinazohusiana na ukiukwaji wa haki za kibinadamu kuhusiana na Maambukizi ya Virusi vya UKIMWI.
Mahakama iliamua kwamba hatua zilizochukuliwa na FO zilikiuka sheria ya Kuzuia na Kudhibiti UKIMWI (HAPCA) na kwamba kitendo cha kufichua hali halisi ya kiafya ya PMM (Sio jina lake halisi) kwenye group la WhatsApp bila ridhaa yake ni kinyume na sheria.
Aliyejulikana kama PMM kwenye nyaraka za kesi hiyo aliiambia Mahakama kwamba alihisi hali ya kukataliwa na wenzake kwenye jamii kiasi kwamba hana uhuru wa kutoa maoni yake popote na anasema alipomuuliza Rafiki yake sababu za kutangaza kuwa ana UKIMWI, Mshtakiwa alimjibu vyote anavyosema ni upuuzi.
Aliyeshtakiwa hakuwahi kuonekana wala kuwasilisha jibu lolote la madai dhidi yake licha ya kuamriwa kulipa kiasi hicho cha fedha na kesi yake kuendelea kuskilizwa bila ya yeye kuwepo Mahakamani.