Serikali ya Ukraine inapanga kuweka kituo cha nafaka mjini Mombasa – Rais Ruto
Rais wa Kenya William Ruto sasa anasema serikali ya Ukraine inapanga kuweka kituo cha nafaka mjini Mombasa kama sehemu ya hatua kubwa ya kukabiliana na uhaba wa chakula nchini Kenya na maeneo mengine ya Afrika Mashariki.
Ruto ambaye alikutana na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyy pembezoni mwa mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mjini New York nchini Marekani siku ya Jumanne alisisitiza uungaji mkono wake wa suluhu la amani kwa mzozo wa Russia na Ukraine.
“Huko New York, Marekani nilifanya mazungumzo na Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskyyambaye aliazimia kuanzisha kituo cha nafaka katika Bandari ya Mombasa ili kukabiliana na uhaba wa chakula Afrika Mashariki,” Ruto alisema Jumanne.
“Kenya inatetea utatuzi wa amani wa mzozo wa Urusi na Ukraine ili kurejesha utulivu, kupunguza mateso ya watu na kukomesha uharibifu wa mali.”
Katika ratiba yake ya Jumanne, Rais Ruto pia alifanya mazungumzo na Rais wa Benki ya Dunia Ajay Banga.