Mbwa Wa Rais Joe Biden Atimuliwa Ikulu Kwa Kuwang’ata Wafanyakazi Na Walinzi
Mbwa wa familia ya Rais Joe Biden wa Marekani, Commander ametimuliwa ikulu kwa kile kilichoelezwa kuwa ni mfululizo wa matukio ya kuwang’ata wafanyakazi wa ikulu wakiwemo walinzi wa rais huyo.
Taarifa za kuondolewa kwa mbwa huyo, zimethibitishwa na msemaji wa mke wa Biden, Jill Biden, Elizabeth Alexander.
Inaelezwa kwamba wiki iliyopita, mbwa huyo alimng’ata mmoja kati ya walinzi wa siri wa Biden na kusababisha apewe matibabu ya dharura.
Inaelezwa kuwa tukio hilo ni la 11 la mbwa huyo kuwang’ata watumishi mbalimbali wa ikulu.
“Rais na mkewe wanajali sana kuhusu usalama wa watu wanaofanya kazi White House na wale wanaowalinda kila siku,” alikaririwa msemaji huyo katika taarifa kwa umma iliyotolewa jana, Jumatano.
Taarifa hiyo haijaeleza wazi mahali alipo mbwa huyo kwa sasa ingawa inaelezwa kwamba hatarudishwa ikulu.