Wapelelezi wa Umoja wa Mataifa wameihimiza Urusi kukiri kuhusika na shambulizi la kombora
Wapelelezi wa Umoja wa Mataifa wameihimiza Urusi kukiri kuhusika na shambulizi la kombora kwenye kijiji kimoja cha Ukraine lililowauwa raia 59.
Wameitaka Urusi ifanye uchunguzi wa wazi kuhusu kilichotokea, itoe fidia kwa waathiriwa na iwawajibishe waliohusika.
Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa Ufuatiliaji wa Haki za Binaadamu nchini Ukraine umesema katika ripoti iliyochapishwa leo kuwa ina ushahidi wa kutosha kwamba kombora la Urusi la masafa mafupi huenda lilisababisha mlipuko huo katika kijiji cha Hroza mnamo Oktoba 5.
Familia zote ziliangamia wakati zikiwa katika hafla ya kumuaga askari wa eneo hilo aliyeuawa wakati akipigana na askari wa Urusi. Mlipuko huo uliwauwa wanawake 36, wanaume 22 na mvulana wa umri wa miaka minane.
Source: dw_kiswahili